Kielezi Cha Tungo
()
About this ebook
Kielezi cha Tungo ni kitabu kinachojadili kwa mapana namna ya kuandika tungo mbalimbali. Hiki ni kitabu cha kipekee ambacho kimeangazia aina mbalimbali za tungo kwa kina. Mwandishi huyu anatoa mifano maridhawa katika kila utungo anaoushughulikia. Kina sehemu zinazoshughulikia maana na aina za insha, tungo amilifu, tungo za kifasihi, ufahamu na ufupisho. Aidha amelijadili kwa mapana swala la uakifishi. Kitabu hiki kitawafaa sana wanafunzi na walimu wa shule na vyuo mbalimbali pamoja na watu wanaokumbana na tungo za namna mbalimbali katika shughuli zao.
Related to Kielezi Cha Tungo
Related ebooks
Tungo Zetu: Msingi wa Mashairi na Tungo Nyinginezo Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsDarubinii ya Sarufi Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsFasihi Simulizi: Kwa Shule Za Sekondari Rating: 3 out of 5 stars3/5Maneno na Aina za Maneno Rating: 5 out of 5 stars5/5Mashairi Rahisi:Mazoezi Na Majibu Kielelezo Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsMachozi Yamenishiya Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsUjasusi Ni Nini? Na Je Majasusi Wanafanya Kazi Gani Hasa? Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsAfisa Usalama Wa Taifa Ni Mtu Wa Aina Gani? Na Anafanya Nini? Rating: 4 out of 5 stars4/5Miaka Miwili Ya Urais Wa Magufuli: Safari Ya Matumaini Au Nyota Iliyofifia? Rating: 1 out of 5 stars1/5Ramani ya Kiswahili Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsJinsi ya Kusali & Kuongea na Yahweh Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsUtatu Mtakatifu Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsUfufuo & Uchukuo Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsYisrael Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsMilenia ya Kristo Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsMafundisho ya Utajiri Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsVile Unavyopaswa Kuwa: kujitambua na kuchukua hatua: Kujitambua, #1 Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsMafundisho ya Ndoa Rating: 0 out of 5 stars0 ratingsMwana-Adam ni Nani Naye ni Nini Mungu Amkomboe: Chuo cha Kwanza, #1 Rating: 0 out of 5 stars0 ratings
Reviews for Kielezi Cha Tungo
0 ratings0 reviews
Book preview
Kielezi Cha Tungo - Focus Publishers
Kielezi cha Tungo
Kitabu hiki kimetolewa kwa mara ya kwanza 2007 na Focus Publishers Ltd
S.L.P 28176
00200 Nairobi, Kenya
barue:focus@africaonline.co.ke
© Timothy M Arege 2007
Haki zote zimehifadhiwa. Hairuhusiwi kuiga, kunakili, kupiga chapa au kukitoa kitabu hiki kwa jinsi yoyote bila idhini ya Focus Publications Ltd
ISBN: 9966-001-096-3
Kimepigwa chapa na
English Press Ltd.
P. O. Box 30127
Nairobi, Kenya
Contents
Foreword
SHUKRANI
UTANGULIZI
SEHEMU I
MAANA YA INSHA NA MASUALA YA KIMSINGI KUHUSU INSHA
Maana ya Insha
Masuala ya Kimsingi Kuhusu Insha
SEHEMU II
AINA ZA INSHA
Insha Simulizi
Insha ya Mjadala/Mdahalo
Insha ya Ufafanuzi/Fafanuzi
Insha Elezi/ya maelezo
Insha ya Methali
Insha ya Mdokezo
Insha za Picha
Insha ya Mawazo
Insha ya Wasifu
Insha za Kitawasifu
SEHEMU III
TUNGO AMILIFU
Maana ya Tungo Amilifu
Risala
Maagizo/Maelekezo
Ujumbe Mfupi/Ujumbe wa Rununu
Hotuba
Dayolojia/Mazungumzo
Barua
Barua za Kirafiki/Kidugu
Barua Rasmi
Aina za Barua Rasmi
Barua kwa Vyombo vya Habari
Barua za mialiko
Mialiko Rasmi
Mialiko isiyo Rasmi
Utumaji wa Barua na Jumbe Nyinginezo
Mdahilishi
Kumbukumbu
Mpangilio wa Kumbukumbu
Usambazaji wa Kumbukumbu
Ripoti
Viungo vya Ripoti Amali
Ripoti za kawaida
Ripoti/Makala za Magazeti
Ripoti/Makala za Televisheni
Ripoti/Makala za Redio
Ushi/Kitawasifu
Memo
Shajara
Mahojiano
Matangazo
Hojaji
Notisi
Resipe
Orodha
Fomu
Tahakiki
Tahariri
Ratiba
SEHEMU IV
TUNGO ZA KIFASIHI
Utangulizi
Utungaji wa Hadithi Fupi
Urefu
Uasili
Wahusika
Mandhari
Msuko/Ploti
Migogoro
Muundo
Wakati
Anwani
Utungaji wa Riwaya
Maana ya Riwaya
Maudhui na Dhamira
Wahusika
Migogoro
Usimulizi
Mandhari
Msuko
Lugha
Anwani
Utungaji wa Tamthilia
Maana ya Tamthilia
Maudhui
Wahusika
Lugha
Muundo
Anwani
Utungaji wa Mashairi
Maana ya Shairi
Wazo
Mkabala wa Kuandikia
Lugha
Aina ya Shairi
Anwani
SEHEMU V
UFAHAMU NA UFUPISHO
Ufahamu
Aina za Ufahamu
Ufupisho
Manufaa ya Ufupisho
Mbinu za Kufupisha Habari
Janga la Ukimwi
SEHEMU VI
Uakifishi
Maana ya Uakifishi
Nukta (.)
Alama ya kuuliza/kiulizi (?)
Alama ya hisi (!)
Koma/Mkato (,)
Nukta na Mkato/Semi-koloni (;)
Nukta mbili/koloni (:)
Alama za Nukuu (
)
Kistari Kirefu (—)
Kistari Kifupi (-)
Kinyota (*)
Mabano Mduara ( )
Mabano Mraba [ ]
Nukta za Dukuduku (…)
Mkwaju/Mshazari (/)
Herufi Kubwa
Herufi za Mlazo/Maandishi ya Mlazo/Italiki
Herufi Nzito
Kupiga Mstari
Ritifaa (‘)
Marejeleo
Faharasa
Foreword
Kwa heshima ya marehemu
Jay Kitsao
Richard S. Mgullu
na
Tom Machuma
Naikumbuka, hori yangu maarufu
Menieleka, nilipokuwa dhaifu
Ikanipeka, pasipo na masumbufu
Nilikotaka, hori yangu menikifu.
Japo safari, iwe fupi au ndefu
Iwe bahari, ni shwari au chafu
Yenye hatari, na wingi wa takilifu
Hupita hori, japo moyo una khofu.
(Boukheit Amana, 1982)
SHUKRANI
Uandishi wa kitabu hiki umekamilika kwa msaada wa watu wengi walionifaa kwa namna mbalimbali katika hatua mbalimbali za utunzi wake. Ni muhali kuwataja wote hapa kwa majina ingawa fadhila zao mbalimbali ziliniwezesha kupiga hatua nilipokuwa nauandaa mswada wa kitabu hiki.
Namshukuru Dkt. K.W. Wamitila kwa ushauri wake mwingi na himizo zisizoisha kuhusu umuhimu wa kuchangia taaluma ya Kiswahili kwa maandishi. Ni Muhali kusahau himizo na ushauri wa Prof Paul Ogula na Dkt. Winston Akala ambao hawaishi kunichochea kuandika kila tunapokutana.
Naomba kutoa shukrani zangu za dhati kwa Abeid S. Abdallah, Naomi Moraa, Biasha Salim, Lucy Maina, Jacob Mogoa, Alice Kiai, John Nyambega, Anastasia Mallya, Assumpta Matei na Joy Walucho walionifaa kwa namna mbalimbali.
Hata hivyo, ningependa kubainisha kuwa endapo kuna kasoro zozote katika kitabu hiki, ni zangu mwenyewe.
Timothy M. Arege
Idara ya Kiswahili,
Chuo Kikuu Katoliki
Novemba 6, 2006
UTANGULIZI
Kielezi cha Tungo ni kitabu ambacho nimekiandika baada ya kuona pengo lililopo katika uwanja wa Kiswahili tarafu ya tungo. Vipo vitabu mbalimbali vinavyozungumzia uandishi wa insha ila niliona nizame ndani zaidi kuliko vilivyofanya vitabu vilivyopo. Natumai kuwa kitabu hiki kitachangia katika ufundishaji na usomaji unaohusu tungo mbalimbali.
Kitabu hiki nimekigawa katika sehemu sita. Sehemu ya kwanza inatoa maelezo ya kijumla kuhusu uandishi wa insha yoyote. Maelezo haya ni ya kimsingi na hivyo yatamfaa mtumiaji wa kitabu hiki kwa kuwa kioo cha kusomea sura zinazofuatia.
Sehemu ya pili inahusu aina za insha. Aina hizo mbalimbali zimejadiliwa na mfano wa kila aina kutolewa. Sehemu hii nilipendelea sana iitwe ‘Mikabala ya Kiutunzi’ au ‘Mitindo ya Kiutunzi’. Hata hivyo, nimetumia anwani ‘Aina za Insha’ kwa sababu ya mazoea yaliyopo na kwa sababu ya wanafunzi wetu wa shule za upili ambao sikutaka wakanganyike.
Sehemu ya tatu inashughulikia tungo amilifu. Hapa nimejitahidi kuangazia kwa mapana aina mbalimbali za tungo amilifu na mitindo mbalimbali iliyopo katika tungo zenye zaidi ya mtindo mmoja kama vile uandishi wa barua rasmi. Sehemu ya nne imeangazia kuhusu jinsi ya kuandika tungo za fasihi andishi. Niliona nizijumuishe tungo hizi katika kitabu hiki kwa sababu hizi vilevile ni tungo zinazoandikwa na zenyewe huwa na kanuni zake.
Sehemu ya tano inashughulikia ufahamu na ufupisho. Hizi ni tungo zenye kupima kiwango cha uelewa na mbinu za mtu kuyaeleza upya aliyoyasoma au aliyoyasikia kulingana na maagizo aliyopewa.
Sehemu ya sita, ambayo ndiyo ya mwisho kabisa, inahusu uakifishi. Uakifishi si aina ya utungo lakini ni suala muhimu katika kuandaa aina yoyote ile ya tungo. Sehemu hii inazungumzia kwa mapana matumizi ya herufi kubwa na viakifishi mbalimbali. Nimejitahidi kutumia mifano kutoka tungo za waandishi wetu wa Kiswahili hapa na pale kusudi niwakutanishe humu na pia wapate kutangamana na wasomaji wa kitabu hiki japo kidogo tu. Aidha, nimetoa mifano sahihi na isiyo sahihi katika utumiaji wa viakifishi. Natumai itamsaidia msomaji kuelewa suala la uakifishi zaidi.
Kitabu hiki pamoja na kwamba huenda kikawafaa wanafunzi wa viwango mbalimbali vya masomo zaidi hasa kwa ajili ya kuiandalia mitihani yao, kwa kiasi kikubwa nimejaribu kuyajadili masuala na vipengele mbalimbali nilivyoshughulikia kwa kuvipa mtazamo mpana. Nimezingatia baadhi ya mambo ambayo yanakwenda na mazingira ya kikazi ili kuuweka uandishi wa tungo katika mazingira yake halisi kama vile hali ya kikazi. Kwa mfano, nimezingatia mambo kama vile ujiandaaji na uandaaji wa mahojiano kabla ya mahojiano yenyewe pamoja na jinsi ya kuyakabili mahojiano unapohoji au kuhojiwa. Aidha, nimeliangazia kwa mfano suala la maandalizi kabla ya kumbukumbu. Nilihisi ipo haja ya wanafunzi kufahamu mazingira na taratibu zinazozunguka uandishi wa tungo badala ya kuandika tungo hizi kwa kuiga miundo na mitindo yake kikasuku tu. Niliona kuwa maelezo hayo yatawafaa katika harakati zao baada ya masomo wanapokwenda kutafuta kazi au kuitenda kazi yenyewe. Jambo lingine nililoona ni kuwa watu wanaofanya kazi wamesahaulika nami nikaona nikipe kitabu hiki mtazamo mpana utakaokidhi haja zao pia. Kwa ufupi, nilitaka kuwalenga ndege wengi kwa jiwe hili hili moja.
Ni matumaini yangu kuwa kitabu hiki kitachangia katika kulijaza pengo japo kidogo katika uandishi wa tungo.
Timothy M. Arege Idara ya Kiswahili,
Chuo Kikuu Katoliki (Nairobi.)
Novemba 6, 2006
SEHEMU I
MAANA YA INSHA NA MASUALA YA KIMSINGI KUHUSU INSHA
* * *
Maana ya Insha
Insha ni utungo ulioandikwa. Utungo huu huweza kuhusu mada au suala lolote na huweza kuandikiwa kwa njia mbalimbali na katika miktadha mbalimbali kutegemea na matakwa ya anayeuandika.
Katika muktadha wa shule, insha huwa ni matini fupi ambayo huandikwa kama zoezi la kutahiniwa na mwalimu.
* * *
Masuala ya Kimsingi Kuhusu Insha
Katika sehemu hii nitajadili kuhusu masuala ya kimsingi ambayo ni uti wa mgongo kwa mtunzi wa insha yoyote ile. Neno insha katika muktadha huu lina maana pana. Tutalitumia kurejelea mitungo mbalimbali kama ile inayotungwa na wanafunzi wa shule za msingi na za upili na vilevile ile inayoandikwa na wanafunzi wa vyuoni.
Masuala yanayojadiliwa katika sehemu hii ni ya kijumla zaidi. Yaani, ni masuala ambayo yanasaidia katika kuandika aina mbalimbali za tungo katika viwango mbalimbali vya taaluma ya elimu.
Masuala hayo ni:
Anwani/Kichwa/Mada
Anwani ni muhimu sana katika aina yoyote ile ya utungo. Insha isiyokuwa na anwani ni kama mtu asiyekuwa na jina. Jina ndilo humtambulisha mtu na kumpambanua kutoka kwa wengine. Insha nayo hutambulika kupitia kwa anwani yake. Anwani ya insha humwezesha msomaji kutambua jambo ambalo linaandikiwa na hivyo kumwezesha kupata wazo la kijumla kuhusu insha inayohusika na wakati mwingine mwelekeo wa insha.
Kichwa cha insha hakifai kuwa kirefu. Maneno sita au chini ya haya yanatosha kuunda kichwa cha insha. Kichwa cha insha si maelezo marefu au masimulizi ya namna fulani. Kinaweza kuwa hata cha neno moja mradi neno hilo liwe linaakisi kinachoshughulikiwa katika insha husika. Kichwa cha insha kinafaa kuwa chenye mvuto. Si rahisi kulitimiza hili mpaka uwe una tajriba kubwa katika uandishi. Kichwa chenye mvuto humtia mshawasha msomaji wa insha na kumpa hamu ya kuisoma insha. Kichwa hicho lazima kioane na yale yanayoshughulikiwa katika insha.
Kichwa cha insha au mtungo kinaweza kuandikwa baada ya kuianza insha au kikaandikwa baada ya kuikamilisha insha maana huu ndio wakati ambapo mwandishi atakuwa ameuona vizuri mkondo wa insha yake. Mtindo huu wa pili unafaa zaidi katika tungo zinazofanyiwa utafiti kama zile wanazoandika wanafunzi wa vyuo vikuu. Kwa kuwa mwanafunzi wa shule ya upili atahitajika kuandika insha yake katika kipindi kifupi cha wakati, kuna hatari ya kusahau kuiandika anwani ya insha yake endapo atahiari kuiandika baada ya kuukamilisha mtungo wake.
Wazo kuu
Unapoandika insha huwa una lengo fulani. Huwezi kuandika insha bila kuwa na lengo. Mwandishi yeyote yule huwa ana wazo kuu analotaka kuliwasilisha kwa msomaji au wasomaji wake. Wazo hilo kuu vilevile hujulikana kama wazo la kimsingi. Wazo hilo kuu wakati mwingine huweza kumulikwa katika kichwa cha insha.
Insha nzuri inafaa kudokeza moja kwa moja, kwa namna moja au nyingine, jambo ambalo mwandishi wa insha analishughulikia. Hatua ya pili ni kulieleza wazo hilo na hatimaye kulitolea hitimisho. Hatua hizi tatu husaidia kuujenga mtazamo wa mtunzi kuhusu jambo analolizungumzia. Mtu anapoisoma hadithi yako na kushindwa kulipata wazo kuu, ina maana kuwa hukufanikiwa kulidhihirisha vizuri hilo wazo kuu.
Ni muhimu basi kuwa na wazo kuu tayari akilini mwako kabla ya kuanza kuiandika insha yako.
Taja/eleza wazo kuu kikamilifu mwanzoni mwa insha yako na ikiwezekana katika anwani yako.
Endeleza wazo lako katika sehemu ya kati.
Hitimisha baada ya kuyafafanua yote uliyodhamiria au kulingana na idadi ya maneno au urefu wa nafasi uliyopewa. Hakikisha unataja/unalidokeza wazo kuu katika sehemu hii.
Hakikisha kuwa kila insha unayoandika inajengwa kutokana na wazo kuu na kuwa chochote unachoandika kuhusu wazo kuu kinasaidia kumpambanulia msomaji kwa uwazi na kwa njia inayofaa kuhusu wazo hilo.
Utangulizi
Insha au utungo wowote ule huwa na sehemu tatu – utangulizi/mwanzo, mwili/kati, na hitimisho/mwisho. Mara nyingi utangulizi huwa ndio sehemu ngumu zaidi kuandika katika insha. Utangulizi ni mojawapo ya sehemu muhimu sana katika uandishi wa insha kwa kuwa ndio ambao humpa msomaji athari ya kwanza na labda ya kudumu. Huweza kumfanya avutiwe nayo au akinai pindi aanzapo kuisoma. Sehemu hii ndiyo huonyesha hisia na mtazamo wa mwandishi pamoja na toni. Toni yaweza kuwa yenye urasmi au usorasmi, dhati au yenye kuchekesha, kudharau/kubeza au kuheshimu, kukejeli, kudadisi, n.k. Utangulizi ni muhimu sana katika kuonyesha hisia hizi.
Hii haimaanishi kuwa mwanafunzi autumie muda wake mwingi kuushughulikia utangulizi mzuri hivi kwamba atapoteza nusu ya muda aliopewa kuwazia jinsi atakavyoiandika aya ya kwanza.
Udokezaji moja kwa moja wa wazo kuu au lengo la insha aghalabu huwa ndio mwanzo/utangulizi mzuri. Njia nyingine ya kukuhakikishia mwanzo mzuri wa insha yako ni kutumia kisa chenye mvuto au mfano ambao unaoana na jambo linalojadiliwa. Aidha, unaweza kuuliza swali lenye kudara ambalo linaweza kujibiwa katika insha yako. Unaweza pia kutumia takwimu zenye kushangaza au data nyingineyo ya kweli. Namna nyingine ya kutoa kauli isiyo ya kawaida ambayo itawavutia wasomaji ni kurejelea/kueleza tajriba ya mwandishi kuhusiana na jambo linalojadiliwa, ufafanuzi wa jambo linaloshughulikiwa au kutoa maelezo ya usuli ambayo yatamfaa msomaji. Wakati mwingine mbinu mbili au zaidi kati ya hizi huweza kutumiwa.
Katika insha/utungo mfupi (kwa mfano majibu ya maswali ya fasihi katika mtihani) utangulizi mfupi ndio unaofaa zaidi.
Je, ni mambo gani unayofaa kuyaepuka unapoandika/ andaa utangulizi wako?
Usifanye sentensi ya kwanza katika utungo wako kutegemea anwani ya insha ili kuleta maana. Kwa mfano ikiwa insha yako ina anwani: Visa vya Uhalifu, usianze insha yako na sentensi kama Visa hivi vimeleta…
Anza aya ya ufunguzi kwa sentensi kamilifu ambayo inajitosheleza yenyewe kimaana.
Usiufanye utangulizi wako kuonekana kuwa ni urudiaji tu wa anwani. Kwa mfano ikiwa unaandika insha yenye anwani Jumuiya ya Afrika Mashariki Itafaa Wananchi,
sentensi kama vile Jumuiya ya Afrika Mashariki itawafaa wananchi wa mataifa matatu yanayojenga umoja huo
haitafaa.
Aidha, usianze sentensi yako na ukosefu wa uhakika kama vile Sielewi kwa kina umuhimu wa jumuiya ya Afrika Mashariki ingawa nitajitahidi kuueleza
.
Mwili/Kati
Sehemu ya kati ndiyo hulifafanua swala linaloandikiwa insha. Sehemu hii lazima ioane na ile ya utangulizi. Wazo lililo katika utangulizi hufafanuliwa hapa. Sehemu hii ndiyo pia huiandalia sehemu ya hitimisho. Hitimisho hutegemea mkondo wa mjadala katika sehemu hii. Utaona kuwa sehemu ya utangulizi huiandalia ya kati nayo ya kati huiandalia ile ya hitimisho. Sehemu hizi huwa kama vipande vinavyojenga mkufu.
Katika sehemu ya kati, unaweza kutoa mifano mwafaka kulifafanua au kulipambanua swala unaloliandikia. Aidha unaweza kutumia maswali ya balagha ili kuchochea fikra ya msomaji wa utungo wako. Pia unaweza kuteka makini ya msomaji wa utungo wako kwa kutumia taharuki. Hizi ni baadhi ya mbinu ya kukusaidia kuleta mvuto katika insha yako.
Daima kumbuka kuwa sehemu hii ndiyo yenye kushughulikia suala unaloliandikia na hivyo habari zote muhimu kuhusu swala hilo lazima zishughulikiwe hapa.
Hitimisho/Mwisho
Njia iliyozoeleka na inayotumiwa zaidi katika kuhitimisha insha ni ile ya kutoa muhtasari wa yale ambayo yameandikiwa katika insha. Wanafunzi wengi huushikilia sana mtindo huu kwa kufikiri kuwa insha inahitimishwa kwa njia hii tu.
Nyingi ya tungo ambazo ni fupi mno hazihitaji mhutasari wa yale yaliyoandikiwa. Hata hivyo, iwapo utahisi kuwa muhtasari utafaa katika kuhitimisha insha yako, usiyarudie tu mambo kwa maneno yale yale uliyoyatumia awali. Ikiwa unataka kulirejelea tena wazo kuu la insha yako, lieleze kwa maneno mengine tofauti na kwa mkazo zaidi kuliko ulivyofanya katika sehemu nyingine za insha yako. Iwapo insha yako ina urefu wa kutosha na utata unaohitaji muhtasari, hakikisha kuwa unautoa muhtasari huo.
Wakati mwingine tahadhari au ushawishi kuhusu mtazamo wako au kuchukuliwa kwa hatua fulani huweza kuwa njia nzuri ya kuhitimisha insha iwapo unaona kuwa hilo litatimiza lengo lako.
Unaweza kutumia kisa kinachovutia au mfano kabambe au maelezo ambayo yanasisitiza wazo kuu katika kuhitimisha. Mtindo wowote ule utakaohiari kuutumia, ni sharti sehemu ya mwisho ya insha yako iwe na mantiki – yaani iwe inatokana na yale ambayo yameshughulikiwa katika insha yako. Inahitaji kutilia mkazo wazo kuu katika insha yako na isiwe maelezo/habari ambazo zinavuruga makini ya msomaji
na kumtenga na lengo la insha yako.
Hitimisho halifai kuwa maelezo ya kijumla tu. Maelezo ya aina hii si tofauti na mihtasari iliyofupishwa ambayo haina thamani yoyote.
Aidha, lisiwe lina masikitiko au yenye kutaka kuhurumiwa kwa kuwa huna habari kuhusiana na jambo unaloliandikia au kwamba unakosa uwezo wa kuandika insha nzuri kuhusiana na jambo ulilotakiwa kulishughulikia.
Hitimisho huhitaji kuhitimisha mawazo yako pasi kumwacha msomaji akihisi kuwa muda wako uliisha au kwamba ulifikia idadi ya maneno uliyohitajika kuyatumia au kwamba ulifika mwishoni mwa ukurasa na ukaamua kuacha kuandika.
Haina haja kuandika Mwisho
au Tamati
unapofika mwisho wa insha yako. Mtahini au msomaji ataweza kuona kuwa umefika mwisho kwa kuhitimisha kuzuri utakakofanya.
Uteuzi mzuri wa maneno
Mwandishi yeyote yule haandiki tu bali hufanya uteuzi mzuri wa maneno atakayo kuyatumia na vilevile kuutumia ufundi mkubwa kuyaunga maneno hayo kujenga sentensi na aya ili kufanikisha mawasiliano. Aina za maneno ndizo hutufanya kuzungumzia kuhusu aina ya lugha k.v. lugha rasmi au isiyo rasmi, lugha sanifu au ya mitaani (isiyo sanifu), n.k. Ilimradi kila utungo una lugha yake inayoteuliwa kuuandika.
Kwa jumla uteuzi mzuri wa lugha ni ule unaofumbata hasa kile kinachoelezewa, yenye kufaa katika muktadha ambapo imetumiwa na yenye kuleta udhahiri unaohitajika katika utungo. Kimsingi lugha hiyo hutakiwa kuwa sanifu. Si neno hata kama itakuwa lugha ya kawaida au lugha ya kitamathali.
Neno linalogonga ndipo sharti liwe lenye kutoa maelezo yanayohitajika hasa – siyo lenye kukaribia au kushabihiana na au lenye maana karibu sawa na ile inayokusudiwa. Ikiwa unalenga maelezo ya kijumla, neno la jumla litakuwa bora. Ikiwa unalenga maelezo mahususi neno maalum litafaa. Usiseme ‘fenicha’ ukilenga kusema ‘sofa seti’ wala ‘stuli’ ikiwa unalenga ‘fenicha’. Wanafunzi aghalabu huwa na tatizo la kuyapambua baadhi ya maneno kama vile ila – hila, kwa sababu – kwa minajili, mbali na - bali, nadharia – nadhari, n.k. Zipo kamusi za maneno yanayotatanisha ambazo huweza kumsaidia mwanafunzi kukabiliana na tatizo hili.
Neno linalogonga ndipo/sahihi huwa lina maana tambuzi, yaani maana yake ya kimsingi, na vilevile maana kimatilaba sahihi. Yapo maneno mengi yaliyopewa maana nasibishi katika lugha na ni wajibu wako kufahamu maana hizo mbalimbali ili uweze kuyatumia maneno hayo inavyostahili.
Ili kuweza kutambua na kuteua neno sahihi kimuktadha, sharti uweze kutofautisha miktadha mbalimbali ya matumizi ya maneno. Yapo maneno yanayokubalika katika kila muktadha; mengine hayakubaliki katika miktadha yote. Tunateua maneno mahususi ya kutumia katika kila muktadha. Kwa mfano hatutumii neno sanduku katika muktadha wa mazishi bali jeneza. Au kwa mfano katika kanisa neno mheshimiwa halitumiwi tunapowataja viongozi wa kidini.
Uteuzi wa neno lazima uwe unaleta umahususi ili kuweza kujenga mvuto na upambanuzi wa jambo linalozungumziwa. Neno lenye umahususi humpambanua mtu mahususi, mahali mahususi au kitu mahususi ambapo neno la